VIEWED 1393 TIMES

Yanga,Yanga, Yanga kwa hakika utaipenda tu, yakwea kwenye usukani wa Ligi Kuu ya Vodacom.
Young Africans Sports Club imedhihirisha kuwa ni moto wa kuotea mbali baada ya kufanikiwa leo kushika usukani wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara baada ya kuichapa timu ya Azam FC mabao 2-0 katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Kikosi cha mauaji cha mholanzi Ernie Brandts kimefanikiwa kuongoza katika msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom kwa kufikisha pointi 26 baada ya kushinda mchezo wa 6 mfululizo na kufuta tofauti ya pointi iliyokuwepo hapo awali dhidi ya watani wa jadi Simba SC.
Kocha Ernie Brandts alipanga kikosi kazi ambacho kilicheza soka la kuvutia tangu mwanzo wa mchezo mpaka mwisho wa mchezo, huku viungo Domayo, Niyonzima na Chuji wakifunika vibaya eneo la katikatiki.
Yanga ilianza kwa kasi mchezo kwa lengo la kupata bao la mapema, lakini kutokuwa makini kwa mshambuliaji Saimon Msuva na Hamis Kiiza walikosa mabao ya wazo dakika 5 za kipindi cha kwanza kwa kupiga mipira nje ya lango la Azam.
Didier Kavumbagu mshambuliaji wa kimataifa kutoka Burundi aliipatia Yanga bao la kwanza katika dakika ya 8 ya mchezo, akimalizia mpira uliopigwa na Mbuyu Twite kukokelewa na mlinzi Aggrey Morris na kumkuta mfungaji Didier aliyekwamisha wavuni na kuhesabu bao la saba katika Ligi Kuu ya Vodacom.
Azam walikuja juu na kutaka kupata bao la kusawazisha lakini umakini wa walinzi Kelvin Yondan, Nadir Haroub'Cannavaro' ulikuwa kikwazo kwa washambuliaji John Boko na Kipre Tchetche, kwani walikosa maarifa kabisa ya kuitoka ngome ya timu ya Yanga.
Mpira ulikwenda mapumziko Azam FC 0 - 1 Young Africans.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi Yanga ikisaka bao la pili huku Azam ikitafuta bao la kusawazisha, hali iliyopelekea kocha wa Azam Stewart Hall kufanya mabadiliko ya haraka haraka ambayo pia bado hayakuweza kuisadia timu yake.
Hamis Kiiza'Diego' aliipatia Young Africans bao pili dakika ya 69 akimaliza krosi safi iliyopigwa na Athuman Idd 'Chuji' aliyewatoka walinzi wa Azam na kuchonga krosi iliyomkuta mfungaji na kufunga bao zuri la kideoni na kumwacha mlinda mlango wa Azam Mwandini Ali akichupa kudaka mpira bila mafanikio.
Kocha Ernie alimuingiza David Luhende kuchukua nafasi ya Saimon Msuva, mabadiliko haya yalipelekea kuwapoteza kabisa Azam katika mchezo, kwani wachezaji wa Yanga waliweza kumiliki idara zote za mchezo na kufanya kipindi cha pili kuwa kama wanafanya mazoezi kwa kugongeana pasi nyingi.
Dakika ya 90, mwamuzi alishindwa kuipa Yanga penati baada ya Aggrey Morris kumkwatua David Luhende katika eneo la hatari lakini mwamuzi alipeta na kuendelea kuwa mbeleko kwa wana Lamba Lamba.
Mpaka dakika 90 za mchezo za mwamuzi Oden Mbaga zinamalizika, Azam FC 0 - 2 Young Africans.
Washabiki na wanachama walitoka Uwanjani wakiwa na furaha ya ushindi pia kandanda safi lililoonyeshwa na wachezaji wa Yanga, kwani kwa uhakika Azam walipotezana na kuutafuta mpira kwa tochi kipindi cha mchezo.
Yanga imebakisha mchezo mmoja katika mzunguko wa kwanza Ligi Kuu ya Vodacom ambapo itakamilisha kwa kucheza na timu ya Coastal union jijini Tanga siku ya jumapili.
Young Africans: 1.Ally Mustapha 'Barthez', 2.Mbuyu Twite, 3.Oscar Joshua, 4.Nadir Haroub'Cannavaro', 5.Kelvin Yondani, 6.Athuman Idd 'Chuji', 7.Saimon Msuva/David Luhende, 8.Frank Domayo, 9.Didier Kavumbagu, 10.Hamis Kiiza, 11.Haruna Niyonzima
Azam FC: 1.Mwandini Ali, 2.Ibrahim Shikanda, 3.Erasto Nyoni/Haji Nuhu, 4.Said Morad, 5.Aggrey Morris, 6.Jabir Aziz/Ibarim Mwaipopo, 7.Kipre Bolou, 8.Salum Abubakari, 9.John Boko, 10.Kipre Tchetche, 11.Khamis Mcha/Abdi Kassim














