2012-03-30 13:21:44 VIEWED 126 TIMES
Kikosi cha Mabingwa wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati na ligi kuu nchini Tanzania bara, Young Africans imeliteka jiji la Tanga na viunga vyake mara baada ya kuwasili humo, huku wenyeji wa jiji hilo wakiwa na hamu na shauku ya kuwaona mabingwa hao waliotua hapa kwa ajili kusaka pointi 3 muhimu ambazo zitawarudisha katika nafasi ya pili ya msimao wa ligi kuu ya Vodacom.
Young Africans itashuka dimbani kesho katika uwanja wa Mkwakwani majira ya saa 10 alasiri kupambana na timu ya Coastal Union wagosi wa kaya , ikiwa ni mchezo N0: 148 wa ligi kuu ya Vodacom inayoelekea ukingoni.
Coastal Union inayoshka nafasi ya 6 katika msimao wa ligi, imekuwa ikitamba kwa maneno na kejeli nyingi dhidi ya timu ya Yanga huku kocha wake Jamhuri Kihwelu akitishia kuiabisha katika mchezo huo.
Kocha Mkuu wa klabu ya Yanga Kostadin Papic amesema anashukuru wamefika salama, wachezaji wake wamepata mda wa kupumzika na leo jioni watafanya mazoezi mepesi katika uwanja wa mkwakwani kwa ajili ya mchezo huo wa kesho.
Papic amesema hakuna vijana wake wanachokihitaji zaidi ya point 3 hapo kesho na ana imani timu yake itaiubuka na ushindi katika mtanange huo, ambapo Yanga kama itafanikiwa kushinda itafanikiwa kupanda nafasi moja hadi ya pili huku ikiwa na michezo sawa na timu za Simba na Azam zilizo juu katika msimamo wa ligi.
Wapenzi wa Yanga washabiki na wanachama wameshafurika jijini hapa tayari kabisa kusubiri kushuhudia mpambano huo hapo kesho katika dimba la Mkwakwani.
Katika kuelekea katika pambano hilo, wenyeji wa jiji hilo na viunga vyake wameonekana kuliongelea pamabano hilo sehemu zote, dalili zinazoonyesha kuwa watazamaji watakuwa wengi katika mchezo huo
Mungu Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Young Africans














